Ticker

6/recent/ticker-posts

SERIKALI ITAENDELEA KUTOA FEDHA ZA UTEKELEZAJI WA MIRADI-MAJALIWA.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema kuwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwenye sekta zote ikiwemo Afya, Maji, Elimu na Miundombinu ya Barabara.

Amesema hayo leo (Jumamosi, Oktoba 05, 2024) alipozungumza na wakazi wa Mbagala Kizuiani, Temeke jijini Dar es Salaam ambapo yupo kwenye ziara ya kikazi.

Amesema kuwa Serikali ipo imara na imedhamiria kuendelea kuwatumikia watanzania wote. “Niwahakikishie kuwa Rais wetu Dkt. Samia yupo imara na anaupendo kwa Watanzania, dhamira, mipango na mienendo yake ya utawala ipo safi”.

Katika hatua nyungine, Mheshimiwa Majaliwa amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) aende Wilaya ya Temeke na kutembelea viwanda vinavyolalimikiwa kutiririsha maji kwenye makazi ya watu na barabara.

Aidha, amemuagiza Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke Ndg. Jomaary Satura kuhakikisha anatumia fedha za mapato ya ndani kuweka taa za barabarani katika maeneo yote yenye uhitaji.

Pamoja na mambo mengine, Mheshimiwa Majaliwa amekagua maendeleo ya ujenzi wa Hospitali ya ghorofa sita ya Mbagala Rangi tatu ambayo ujenzi wake unatarajiwa kugharimu shilingi bilioni 10.85 na itasaidia kulaza wagonjwa 165.

Ujenzi wa hospitali hiyo utasaidia kuboresha huduma za afya zikiwemo za kibingwa, kutoa huduma ya upasuaji mkubwa, huduma za dharura, kupunguza msongamano uliopo kwa sasa, kuongeza wigo wa utoaji huduma kwa wananchi, kupunguza rufaa zisizo na ulazima na kuhudumia wananchi wa Mbagala na maeneo ya jirani.

Pia, Mheshimiwa Majaliwa alikagua Ujenzi, Upanuzi na Ukarabati wa Daraja na Barabara ya Mivinjeni na Bandari One jijini Dar es salam.

Post a Comment

0 Comments