Ticker

6/recent/ticker-posts

MUSHI AWATAKA WARATIBU WA MRADI WA HEET KUONGEZA KASI YA MCHAKATO WA MANUNUZI

NAIBU Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia (Sayansi,Teknolojia na Ubunifu) Daniel Mushi amewataka waratibu wa mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET),kuongeza kasi ya mchakato wa manunuzi pamoja na kusimamia fedha kwa weledi,ili zifanye kazi iliyo kusudiwa.

Ameyasema hayo leo Oktoba 10,2024 Jijini Dar es salaam wakati alipokutana na waratibu hao kwa lengo la kuwasisitiza kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huo ili ukamilike kwa wakati.

Amesema mradi huo unauhusisha taasisi 22 za elimu ya juu pamoja na elimu kati ambapo zimetengewa fedha zaidi ya shilingi billion 900 za kitanzania za mkopo nafuu kutoka Benki kuu ya dunia kwa lengo la kufanya ujenzi wa miundombinu ya kisasa ya kujifunzia.

Aidha Naibu Katibu Mkuu amesema wanatarajia ugeni kutoka Benki kuu siku zijazo ambao watakuja kwa ajili ya kufanya tathimini ya kati kuhusiana na Maendeleo ya mradi huo ambapo wameona vyema kujiandaa ili wafanye vizuri watakapofika kufanya tathimini hiyo.

Amesema mradi huo umelenga kukamilisha mambo mbalimbali ambayo yatasaidia Vijana wengi wanaosoma waweze kupambana katika soko la ajira.

Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi umekusudia kuboresha mazingira ya kujifunzia pamoja na kufundishia ili wasomi watakaopatikana kupitia Mradi huo waweze kukidhi mahitaji ya soko la ajira wanapoajiriwa au kujiajiri.

Post a Comment

0 Comments