Ticker

6/recent/ticker-posts

MKUU WA MISHENI YA UANGALIZI WA UCHAGUZI YA SADC NCHINI MSUMBIJI AENDELEA KUKUTANA NA WADAU WA UCHAGUZI NCHINI MSUMBIJI

Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mkuu wa Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC –SEOM) nchini Msumbiji, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume ameendelea kukutana na wadau mbalimbali wa uchaguzi mkuu wa Msumbiji unaotarajiwa kufanyika tarehe 09 Oktoba 2024.

Mhe. Dkt. Karume kwa nyakati tofauti leo tarehe 05 Oktoba 2024 jijini Maputo, amekutana na kufanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri la Msumbiji, Mchungaji Augusto Pedro na Mkurugenzi wa Kituo cha Demokrasia na Haki za Binadamu (CDD), Prof. Adriano Nuvunga.

Katika mazungumzo yake na viongozi hao, Mhe. Dkt. Karume pamoja na mambo mengine aliwaeleza lengo la Misheni hiyo ya SADC kuwa ni kuangalia uchaguzi kwa mujibu wa kanuni na miongozo ya uchaguzi ya SADC iliyorekebishwa mwaka 2021 inayozingatia misingi ya haki, usawa na demokrasia.

Ujumbe wa Mhe. Dkt. Karume kwenye mikutano hiyo uliwajumuisha Wajumbe wa Troika kutoka Tanzania, Zambia na Malawi, Sekretarieti ya SADC akiwemo Mkurugenzi wa Organ , Prof. Kula Ishmael Theletsane na Wajumbe wa Baraza la Ushauri wa masuala ya Uchaguzi la SADC (SEAC). Wajumbe wa Troika kutoka Tanzania walioshiriki ni pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushiriano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaibu Mussa na Mshauri wa Rais masuala ya Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Sofia Mjema.

Vilevile, Mhe. Dkt. Karume amepokea taarifa kutoka kwenye Kamati ya Uandishi ya Misheni hiyo kuhusu utekelezaji wa masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na kupokea taarifa kutoka kwa waangalizi wa SADC ambao walisambazwa kwenye majimbo 11 ya uchaguzi nchini humo tangu tarehe 03 Oktoba 2024.

Mhe. Dkt. Karume kwa nafasi yake ya Mkuu wa Uangalizi wa Uchaguzi ya SADC ameendelea kukutana na viongozi wa Serikali na wadau mbalimbali wa uchaguzi ambapo hadi sasa amekutana na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Msumbiji (CNE), Mabalozi wa Nchi za SADC waliopo Msumbiji, Waziri wa Mambo ya Nje wa Msumbiji, Kamishna Msidizi wa Jeshi la Polisi la Msumbiji na Mgombea urais wa Chama Tawala cha FRELIMO, Mhe. Daniel Francisco Chapo.
Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mkuu wa Misheni ya Uangalizi wa Uchaguzi ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC –SEOM) nchini Msumbiji, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume akizungumza na Katibu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri la Msumbiji, Mchungaji Augusto Pedro (hayupo pichani) ikiwa ni mwendelezo wa Mkuu huyo wa Misheni ya SADC wa kukutana na wadau mbalimbali wa uchaguzi mkuu wa Msumbiji unaotarajiwa kufanyika tarehe 09 Oktoba 2024. Mazungumzo yao yalifanyika jijini Maputo tarehe 5 Oktoba 2024
Katibu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri la Msumbiji, Mchungaji Augusto Pedro akizungumza na Mkuu wa Misheni ya SADC ya uangalizi wa Uchaguzi nchini Msumbiji, Mhe. Dkt. Karume (hayupo pichani)
Mazungumzo yakiendelea kati ya Mhe. Dkt. Karume (kulia) na Mchungaji Pedro (kushoto)
Mhe. Dkt. Karume akizungumza na Mkurugenzi wa Kituo cha Demokrasia na Haki za Binadamu (CDD), Prof. Adriano Nuvunga katika mkutano uliofanyika jijini Maputo tarehe 5 Oktoba 2024
Mjumbe wa Troika na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Sahibu Mussa akichangia jambo wakati wa mkutano kati ya Mhe. Dkt. Karume na Prof. Nuvunga hawapo pichani.
Mjumbe wa Troika na Mshauri wa Rais masuala ya Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Sofia Mjema akichangia hoja wakati wa Mkutano kati ya Mhe. Dkt. Karume na Mkurugenzi wa CDD, Prof. Nuvunga hawapo pichani
Naibu Mwenyekiti wa Baraza la Ushauri la SADC la masuala ya Uchaguzi naye akichangia jambo

Mjumbe wa Troika ambaye pia ni Balozi wa Malawi nchini Msumbiji, Mhe. Wezi Moyo akichangia jambo. Kushoto ni Mjumbe wa Troika kutoka Zambia, Bw. Lubasi
Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Talha Waziri naye akichangia jambo
Mwenyekiti wa Kamati ya Uandishi wa Taarifa ya Misheni ya SADC, Bi. Shazma Msuya akitoa taarifa kwa Mkuu wa Misheni ya SADC ya Uangalizi wa Uchaguzi nchini Msumbiji, Mhe. Dkt. Karume (hayupo pichani)
Bi. Msuya akiwasilisha taarifa kwa Mkuu wa Misheni, Mhe. Dkt. Karume

Uwasiishaji taarifa ya Misheni ukiendelea

Mhe. Dkt. Karume akiwa katika picha ya pamoja na Katibu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri la Msumbiji baada ya kukamilisha mazungumzo yao

Mhe. Dkt. Karume akiagana na Katibu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri la Msumbiji mara baada ya mazungumzo yao

Mhe. Dkt. Karume akiagana na Mkurugenzi wa Kituo cha Demokrasia na Haki za Binadamu (CDD), Prof. Adriano Nuvunga baada ya mazungumzo yao
Picha ya pamoja

Post a Comment

0 Comments