Ticker

6/recent/ticker-posts

BANDARI YA MTWARA KAMILI KUSHUGHULIKIA SHEHENA YOTE YA KOROSHO





Mtwara. 

Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imetangaza kuwa Bandari ya Mtwara ipo tayari kushughulikia shehena yote ya korosho kwa ajili ya mauzo ya nje katika msimu wa sasa wa uuzaji. 

Hii ni kufuatia agizo la Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwamba bandari hiyo itumike kama njia kuu ya kusafirisha korosho ghafi kutoka mikoa ya kusini mwa Tanzania kwenda katika masoko ya kimataifa. 

Akizungumza alipokuwa katika ziara yake mkoani Mtwara mnamo Septemba mwaka jana, Rais Samia alisisitiza kuwa usafirishaji wa korosho kupitia bandari nyingine unatakiwa upate kibali kutoka kwa Mkuu wa Mkoa. Akizingatia agizo hilo, Meneja wa Bandari ya Mtwara, Ferdinand Nyathi, alisema kuwa bandari hiyo sasa imeboreshwa na ipo tayari kushughulikia shehena yote ya korosho msimu huu.

“Msimu uliopita, baada ya agizo la Rais Samia Suluhu Hassan, tuliweza kusafirisha tani 253,000 za korosho na kushughulikia jumla ya meli 28. Mwaka huu, tumejiandaa zaidi kushughulikia mazao ya korosho. Kwa ufupi, tuko tayari kabisa,” alisema Bw Nyathi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari siku ya Ijumaa.

Maandalizi ya bandari yameimarishwa na upatikanaji wa vifaa vipya, ikiwa ni pamoja na kreni mbili za rununu, mashine ya kushughulikia makasha matupu, “reach stackers”, na Tag Boats za kisasa. Vifaa hivi vimeboresha kwa kiasi kikubwa uwezo wa kuhudumia makontena katika bandari hiyo.

“Vifaa hivi vipya vimetuwezesha kujiweka katika nafasi bora zaidi ya kusafirisha korosho zote ambazo Tanzania itauza nje msimu huu,” alisema Bw Nyathi kwa furaha.

Kwa kuwa msimu wa mauzo ya korosho tayari umeshaanza, makontena takriban 3,700 yapo tayari katika Bandari ya Mtwara kushughulikia usafirishaji wa korosho. Bw Nyathi aliongeza kuwa, kwa ushirikiano na sekta binafsi ambayo inamiliki Maeneo ya Makontena ya Ndani (ICDs), bandari hiyo ina makontena mengine 800 ambayo yanaweza kutumika. Upakiaji wa korosho kwenye makontena unaendelea. 

Maboresho haya katika Bandari ya Mtwara ni habari njema kwa wakulima wa korosho, ambao wameona ongezeko la bei katika minada ya karibuni. Kwa mfano, katika mnada wa kwanza uliofanyika tarehe 11 Oktoba, ulioandaliwa na Chama Kikuu cha Ushirika cha Tandahimba na Newala (Tanecu), tani za ujazo 3,857 za korosho ghafi ziliuzwa kwa bei kati ya Sh4,035 na Sh4,120 kwa kilo. Mnada wa pili uliofanyika tarehe 12 Oktoba, ulioandaliwa na Chama Kikuu cha Ushirika cha Lindi Mwamba (LMCU), uliuza tani za ujazo 6,435 kwa bei kati ya TZS 3,400 na Sh3,865 kwa kilo.

Ili kuvutia zaidi wauzaji nje, Bw. Nyathi alitangaza kuwa bandari hiyo imefuta gharama zote za kuhifadhi makasha yenye korosho kwa msimu mzima wa mauzo.

“Hapo awali, kuhifadhi makasha ilikuwa bure kwa kipindi maalum, na baada ya hapo gharama za kuhifadhi zilianza kutozwa. Hata hivyo, kwa msimu huu, kuhifadhi ni bure kabisa kwa msimu mzima wa korosho,” alieleza.

Bw Nyathi alihakikisha pia kwamba usimamizi wa korosho hautaathiri shughuli nyingine za mizigo katika bandari hiyo, ikiwemo bidhaa kama mkaa na saruji. “Tunatarajia meli tatu zaidi kufika bandarini wiki hii, zikiwa na makontena zaidi,” alisema.

Alisisitiza kuwa Bandari ya Mtwara ipo katika eneo muhimu kijiografia kwa wateja wa TPA katika mikoa ya kusini na nchi jirani, akibainisha kuwa maboresho hayo yamewezeshwa na uwekezaji mkubwa wa serikali katika miezi ya karibuni.

Shilingi Bilioni 157.8 bilioni ziliwekezwa katika ujenzi wa gati mpya yenye urefu wa mita 300 katika Bandari ya Mtwara. Gati hiyo, yenye kina cha maji cha mita 13, inaweza kupokea meli zenye urefu wa hadi mita 230 na kushughulikia meli kubwa zenye uzito wa hadi tani 65,000. Miundombinu mipya inajumuisha eneo la mraba mita 75,807 linaloweza kuhifadhi makasha ya futi ishirini (TEUs) hadi 8,600 kila mwaka.

Uwezo wa kushughulikia mizigo katika Bandari ya Mtwara umeongezeka kwa kiwango kikubwa katika miaka ya hivi karibuni. Katika mwaka wa fedha wa 2022/2023, bandari hiyo ilishughulikia tani milioni 1.629 za mizigo, ongezeko kubwa ikilinganishwa na tani 106,170 zilizorekodiwa katika mwaka wa fedha wa 2018/2019.

Kwa mwaka wa fedha 2023/24, Bandari ya Mtwara ilihudumia tani 1,727,261 na lengo la mwaka huu ni kuhudumia tani 1,7010,000. 

“Tumejipanga kuhakikisha kuwa Bandari ya Mtwara inakuwa lango kuu la usafirishaji wa korosho na mizigo mingine kutoka kusini mwa Tanzania na kwingineko. Lengo letu ni kushughulikia kila shehena kwa ufanisi huku tukiendelea kuvutia biashara zaidi katika bandari hii,” alisema Bw Nyathi.

Kwa uwekezaji unaoendelea na maboresho ya kimkakati, bandari hii inatarajiwa kuchangia kwa kiasi kikubwa katika sekta ya korosho ya Tanzania na ukuaji wa uchumi wa taifa.

Post a Comment

0 Comments