Ticker

6/recent/ticker-posts

WASAJILI WA HATI WASAIDIZI NCHINI WAJIFUA KUTUMIA MFUMO WA e-Ardhi

 



Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeanzisha Mfumo wa e-Ardhi ili kuimarisha utawala bora na uwajibikaji na kuwezesha miamala Usajili wa Hati kufanyika kwa uwazi zaidi na kuongeza usalama wa milki.

Akifungua mafunzo hayo kwa Wasajili wa Hati Wasaidizi wa Mikoa na Wataalam wa TEHAMA Septemba 21, 2024 mkoani Morogoro, Msajili wa Hati kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bw. David Mushendwa  amesema Mfumo wa e-Ardhi  ni umuhimu katika kuboresha utendaji kazi wa sekta ya Ardhi na wamejifunza namna ya kushughulikia migogoro ya ardhi kwa njia ya kidijitali.

“Mfumo wa e-Ardhi unalenga kuboresha taratibu za usajili wa hati miliki kwa njia ya kidijitali, hatua inayotarajiwa kuondoa changamoto za muda mrefu kama ucheleweshaji wa huduma, urasimu, na upotevu wa nyaraka muhimu” amesema Bw. Mushendwa.

Mfumo huo unalenga kuwarahisishia wananchi kufanya miamala ya ardhi kuwa salama na rahisi kufuatilia, ambapo wateja wataweza kufikia taarifa za ardhi zao na kufuatilia hatua za usajili wa hati kwa njia ya mtandao popote walipo hatua inayopunguza adha kwa wateja kusafiri mara kwa mara kwenda ofisi za ardhi na kupunguza gharama za kufanya miamala ya ardhi.

Kwa upande wa Msajili wa Hati msaidizi Mkoa wa Geita Bi. Sophia Chelengwa ameipongeza Wizara na watendaji wote wakiongozwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa juhudi wanazofanya ili kuimarisha sekta ya Ardhi nchini hatua inayoboresha wananchi kupata huduma haraka na kwa ubora. 

Mfumo wa e-Ardhi unatarajiwa kuanza kutumika rasmi nchini kote ambao utasaidia kuweka na kutunza kumbukumbu zinazohusu masuala ya ardhi, kurahisisha kazi na taratibu za utoaji wa milki za ardhi, kuimarisha usalama wa milki za ardhi pamoja na kuondoa ugumu wa kupata taarifa sahihi kwa wakati na kuongeza mapato ya Serikali. 

Mafunzo hayo ni ya siku mbili ambayo yamefanyika kuanzia Septemba 20-21,2024 ili kuhakikisha  wataalamu hao wamepitia  utekelezaji wa Mfumo wa  e-Ardhi katika miamala inayohusisha usajili wa Hati, miamala ya Hati  pamoja na nyaraka mbalimbali za kisheria.

Post a Comment

0 Comments