Ticker

6/recent/ticker-posts

MGODI WA BARRICK BULYANHULU WAKABIDHI VIFAA WEZESHI NA VYA KUFANYIA KAZI KWA WATU WENYE ULEMAVU


Watu wenye mahitaji maalum wakipokea vifaa wezeshi kutoka kwa wawakilishi wa Serikali na mgodi wa Barrick Bulyanhulu katika hafla hiyo.
Baadhi ya watu wenye mahitaji maalum wakiwa katika picha ya pamoja na Maofisa wa Serikali na Mgodi wa Barrick Bulyanhulu katika hafla ya mgodi wa Barrick Bulyanhulu kukabidhi vifaa wezeshi na vya kufanyia kazi kwa watu wenye mahitaji maalum iliyofanyika katika ofisi za kata ya Bugarama.

***

Mgodi wa dhahabu wa Barrick Bulyanhulu uliopo Halmashauri ya Msalala, wilayani Kahama, Mkoani Shinyanga umekabidhi msaada wa vifaa mbalimbali kwa kundi la watu wenye mahitaji maalum 53, kutoka kata za Bulyanhulu na Bugarama, vyenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 25.

Akiongea katika hafla ya kukabidhi vifaa hivyo iliyofanyika katika ofisi za Kata ya Bugarama, Halmashauri ya Msalala, wilayani Kahama, Mwakilishi wa Meneja Mkuu wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu, Lumbu Kambula, amevitaja vifaa ambayo mgodi umetoa kwa wahitaji hao kuwa ni vyerehani, baiskeli, viti mwendo (wheelchairs) ,vifaa vya kuongeza kusikia ,mashine za kuchomelea pamoja na vifaa saidizi kwa watu wenye Ualbino.

Amesema kutolewa kwa vifaa hivyo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa uwajibikaji kwa jamii (Corporate Social Responsibility -CSR) unaotekelezwa na Mgodi wa Barrick Bulyanhulu ambapo walikubaliana na Halmashauri ya wilaya ya Msalala kwamba asilimia 10 ya fedha ya CSR zitumike kwa ajili ya makundi maalumu vikiwemo vikundi vya akina mama,vijana,wazee na watu wenye ulemavu.

“Vifaa wezeshi kwa watu wenye ulemavu na wazee tulivyotoa vina thamani ya zaidi ya shilingi milioni 24 shilingi. Tunatoa shukrani kwa ushirikiano mzuri na viongozi wa ngazi zote katika utekelezaji wa mpango wa maendeleo ya jamii hususani katika kuhudumia makundi maalumu.Tunaomba tuendelee kushirikiana kwa ajili ya kujenga jamii kwa maendeleo endelevu” ,ameongeza Kambula.

Akiongea kwa niaba ya Mkuu wa wilaya ya Kahama, Afisa Tarafa ya Msalala, Victoria Lusana ameupongeza na kuushukuru Mgodi wa Barrick Bulyanhulu kwa kufanikisha kupatikana kwa vifaa wezeshi kwa wazee na watu wenye ulemavu katika kata za Bugarama na Bulyanhulu na kuwatakawanufaika wa msaada huo kuvitumia vifaa hivyo kuvitumia kwa manufaa yaliyokusudiwa.

“Mgodi wa Barrick Bulyanhulu mmekuwa sehemu ya familia ya wakazi wa halmashauri ya wilaya ya Msalala kutokana na ushirikiano ambao mmekuwa mkiutoa kwa jamii. Tunawashukuru kwa kuona umuhimu wa kuyafikia makundi maalumu ambayo kimsingi yanashiriki katika shughuli za maendeleo katika jamii”,amesema Lusana.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Msalala, Judica Sumari amesema mgodi wa Bulyanhulu kwa kushirikiana na halmashauri hiyo wamekuwa wakitekeleza mpango wa uwajibikaji kwa jamii inayozunguka eneo la mgodi katika kata za Bugarama na Bulyanhulu ili kukuza na kuimarisha ustawi wa makundi mbalimbali ya kijamii yaliyopo katika maeneo hayo.

Amewataka wenye ulemavu kuchangamkia fursa ya mikopo ya Serikali ya asilimia 2 ya pato la ndani ambayo imetengwa kwa ajili yao ili waweze kujikwamua kimaisha sambamba na kujiongezea kipato.

Mmoja wa wanufaika wa msaada huo, Daniel Mgata, akiongea kwa niaba ya Wenzake ameshukuru mgodi wa Barrick Bulyanhulu na Halmashauri ya Msalala kwa kuwa na program za kujali watu wenye ulemavu kwa kuwapatia vifaa wezeshi na vifaa vya kufanyia kazi kwa ajili ya kujikwamua kiuchumi.

Mgodi wa Barrick Bulyanhulu mbali na kukabidhi vifaa wezeshi wa wenye mahitaji maalumkupitia fedha za uwajibikaji kwa jamii (CSR) umeweza kutekeleza miradi mbalimbali ya kijamii katika maeneo yanayozunguka mgodi hususani katika sekta ya elimu na afya.
Mwakilishi wa Meneja Mkuu wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu, Lumbu Kambula akiongea wakati wa hafla hiyo ya mgodi wa Barrick Bulyanhulu kukabidhi vifaa wezeshi na vya kufanyia kazi kwa wenye mahitaji maalum iliyofanyika katika ofisi za kata ya Bugarama.Wengine pichani ni Maofisa wa Serikali na Barrick Bulyanhulu
Mwakilishi wa Mkuu wa wilaya ya Kahama, Afisa Tarafa ya Msalala, Victoria Lusana ambaye alikuwa mgeni rasmi akiongea wakati wa hafla hiyo ya mgodi wa Barrick Bulyanhulu kukabidhi vifaa wezeshi na vya kufanyia kazi kwa wenye mahitaji maalum iliyofanyika katika ofisi za kata ya Bugarama
Kaimu Meneja Mahusiano na Mazingira wa Barrick Bulyanhulu, Zuwena Senkondo akieleza mikakati ya mgodi huo kutekeleza programu za uwajibikaji kwa jamii kwa lengo ya kuleta maendeleo kwa wananchi sambamba na kujenga mahusiano mema.
Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Msalala, Judica Sumari akiongea wakati wa hafla hiyo ya mgodi wa Barrick Bulyanhulu kukabidhi vifaa wezeshi na vya kufanyia kazi kwa wenye mahitaji maalum iliyofanyika katika ofisi za kata ya Bugarama. Wengine pichani ni Maofisa wa Serikali na Barrick Bulyanhulu
Mmoja wa wanufaika wa msaada huo, Daniel Mgata (kushoto) akitoa neno la shukrani kwa uwezeshwaji waliopatiwa na mgodi wa Barrick Bulyanhulu.
Watu wenye mahitaji maalum wakipokea vifaa wezeshi kutoka kwa wawakilishi wa Serikali na mgodi wa Barrick Bulyanhulu katika hafla hiyo.
Watu wenye mahitaji maalum wakipokea vifaa wezeshi kutoka kwa wawakilishi wa Serikali na mgodi wa Barrick Bulyanhulu katika hafla hiyo.
Baadhi ya Watu wenye mahitaji maalum katika picha ya pamoja na maofisa wa Serikali na mgodi wa Barrick Bulyanhulu muda mfupi baada ya kukabidhiwa vifaa wezeshi mbalimbali kwa walemavu wenye mahitaji maalum.
Maofisa wa Serikali na Barrick Bulyanhulu katika picha ya pamoja wakati wa hafla hiyo

Post a Comment

0 Comments