Ticker

6/recent/ticker-posts

SERIKALI KUWAJENGEA UWEZO WACHIMBAJI WADOGO KUTUMIA TEKNOLOJIA YA KISASA KATIKA UCHENJUAJI MADINI - WAZIRI MAVUNDE


Na.Samwel Mtuwa - Chunya.


Mwaka 2030 ndio mwisho wa matumizi ya kemikali ya Zebaki katika uchenjuaji na ukamatishaji wa madini ya dhahabu kama mkataba wa kimataifa wa MINAMATA wa mwaka 2013 unavyoelekeza. 


Hayo yamebainishwa na Waziri wa Madini Mhe.Anthony Mavunde Oktoba 29, 2023 wakati anazungumza na wachimbaji wadogo wa madini wa Itumbi Wilaya ya Chunya , Mkoani Mbeya katika ziara maalum ya kikazi.



Waziri Mavunde amesema kuwa moja ya mikakati ya Serikali ni kuwajengea uwezo kitaalam na mashine wachimbaji wadogo wote ili kuachana na uchenjuaji madini kwa kutumia kemikali ya Zebaki na kutumia teknolojia ya kisasa kama vile CIP.


Mhe.Mavunde ameongeza kuwa Serikali inatambua changamoto zote zilizopo kwa wachimbaji wadogo katika upande wa matumizi ya teknolojia kwenye uchimbaji na uchenjuaji madini.



Akielezea kuhusu madhara ya matumizi ya Zebaki kwa wachimbaji wadogo katika uchenjuaji na ukamatishaji madini ya dhahabu , Mhe. Mavunde ameeleza kuwa takribani kiasi cha tani 13.2 hadi 24.4 za kemikali ya zebaki hutumika kwa mwaka ambapo wachimbaji wadogo ndio watumiaji wakubwa wa kemikali hiyo.


Mhe.Mavunde amefafanua kuwa utafiti unaonesha kuwa viwango vya matumizi ya zebaki duniani vinaendelea kukua kila siku katika shughuli za mwanadamu ikiwemo uchomaji wa makaa ya moto na uchenjuaji wa madini ya dhahabu.


Mhe.Mavunde amewaomba wachimbaji wadogo wa dhahabu kuchukua tahadhari kwa kuvaa vifaa kinga wakati wa uchenjuaji na uchomaji wa dhahabu ili kuzuia athari zitokanazo na moshi.


Mhe.Mavunde aliongeza kuwa Serikali imeona kuna umuhimu wa kulinda afya za watanzania na mazingira kwa ujumla iliuridhia mkataba wa kimataifa wa MINAMATA na kuusaini mwaka 2020.


Aidha, Waziri Mavunde aliwapongeza wachimbaji wadogo Mkoa wa Kimadini Chunya kwa kuonesha ushirikiano mzuri na Serikali katika ulipaji wa tozo mbalimbali zitokanazo na mnyororo mzima wa sekta ya madini.


Kwa mujibu wa taarifa ya mwenendo wa sekta madini inaonesha mwaka 2020/2021 Mkoa wa kimadini wa Chunya ulifanya makusanyo ya maduhuli na kuvuka lengo kwa asilimia 159 ambapo mwaka 2021/2022 ulikusanya kwa asilimia 100.85.


*VISION 2030* MADINI NI MAISHA NA UTAJIRI.
;

Post a Comment

0 Comments