Ticker

6/recent/ticker-posts

CHANGAMOTO ZA UCHUKUZI MPAKANI TUNDUMA ZAPATA MUAROBAINI

Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi Prof. Godius Kahyarara amesema Serikali imeanza kushughulikia changamoto za usafirishaji wa mizigo katika kituo cha forodha katika mpaka wa Tunduma ili kurahisisha usafirishaji wa mizigo baina ya Tanzania, Zambia, Zimbabawe na DRC Kongo.

Akizungumza katika kikao kilichowakutanisha wadau wa usafirishaji wanaofanya kazi katika mpaka huo Mkoani Songwe mwishoni mwa wiki Prof. Kahyarara amesema utatuzi wa changamoto hiyo unawashirikisha wadau mbalimbali ikiwemo Trade Mark East Africa na Benki ya Dunia lengo likiwa kuharakisha maboresho yaliyopangwa kufanyika.

“Maeneo muhimu ambayo Serikali imeanza kuyafanyia kazi kwa haraka ni pamoja na kuanza kusimika mashine za ukaguzi wa mizigo na kuboresha mifumo ya tehama itakayosomana kwa taasisi zote zinazotoa huduma mpakan, maboresho hayo yakikamilika tutapiga hatua kwa haraka sana kwenye utoaji wa magari na huduma kwa ujumla’ amesema Prof. Kahyarara.

Prof. Kahyarara amezungumzia faida za maboresho hayo ikiwemo kupungua kwa muda kwa magari yanayopita mpakani hapo, muda wa safari kwa wasafirishaji kupungua, kushuka kwa bei ya bidhaa zinazosafirishiwa kupitia barabara na kuwezesha ufanisi katika Bandari ya Dar es Salaam.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Dkt. Francis Michael ameipongeza Serikali ya awamu ya sita kwa kuongeza nguvu kwenye utatuaji wa changamoto za wasafirishaji zilizopo katika mpaka huo na kusema kukamilika kwa maboresho ambayo yamekuja kwa pamoja na miradi mingine ya upanuzi wa Barabara ya TANZAM kutachagiza maendeleo kwa mkoa wa Songwe.

Naye Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Songwe SSP. Joseph Bukombe amesema kwa sasa Jeshi la Polisi limejiwekea utaratibu maalum wa kusaidia kusaidia uongozaji wa magari kwa kufuata foleni ili kupunguza msongamano kwa watumiaji wa Barabara wanaokwenda mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma kwa kupitia mkoa wa Songwe.

(Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Uchukuzi)


Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara akizungumza na wadau wa Usafirishaji (hawapo pichani) wakati alipokutana nao Mkoani Songwe, mwishoni mwa wiki.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara akimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Dkt. Francis Michael wakati alipomtembelea ofisini kwake Mkoani Songwe, mwishoni mwa wiki.Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara akizungumza na Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Dkt. Francis Michael wakati Katibu Mkuu huyo alipomtembelea Mkuu wa Mkoa huyo ofisini kwake Mkoani Songwe, mwishoni mwa wiki.
Sehemu ya Viongozi wa taasisi za Serikali na Wadau wa Usafirishaji wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara (hayupoo pichani) wakati Katibu Mkuu huyo alipokutana nao Mkoani Songwe, mwishoni mwa wiki.

PICHA NA WIZARA YA UCHUKUZI

Post a Comment

0 Comments